Friday, 4 July 2014

Mtaalam wa Manchester United astaafu baada ya kuitumikia klabu miaka 23

Mkuu wa Kutibu Viungo wa Manchester United, Rob Swire, amestaafu baada ya kuitumikia Klabu hiyo kwa Miaka 23.
Swire, mwenye Miaka 51 na ambaye amekuwa akiongoza Kitengo cha Kutibu Viungo [Physiotherapy] cha Man United tangu Mwaka 1999, alijiunga na Old Trafford Mwaka 1991.
Nafasi ya Swire itachukuliwa na Msaidizi wake Neil Hough ambae yeye mwenyewe ndiye alimteua Miaka 15 iliyopita.
Swire ameamua kwa hiari yake mwenyewe kustaafu na ameeleza: “Si uamuzi rahisi, ni uamuzi mkubwa. Nimekuwa nikifikiria hili kwa zaidi ya Mwaka nikitafuta wakati muafaka nistaafu. Nimefanya kazi hii kwa muda mrefu na bila kuwa na Masaa maalum hivyo unafanya kazi kila wakati, pamoja na Wikiendi na Jioni na kusafiri sana na haikuwa rahisi kwa Familia  yangu.”
SWIRE akimtibu Beckam mwaka 2000
Kadhalika kocha  mstaafu wa Man United, Sir Alex Ferguson, amemsifia sana Swire kwa kusema: “Nakumbuka Rob alipoanza kazi Klabuni, alikuwa ni Kijana mwenye nia ya kazi yake na anaekazania kujiboresha zaidi na kujifunza zaidi. Alikuwa mwaminifu mno. Ni Mtu mzuri na Binadamu safi sana. Sijapata kuwa na tatizo lolote toka kwake.”
Ferguson aliongeza: “Nimefanya kazi na Rob kwa muda mrefu na nasikia fahari kubwa kwa kazi yake. Ameitumikia Klabu vyema na namtakia kila la kheri katika maisha yake ya baadae. ”
Kwa upande wake koche Msaidizi wa Man United, Ryan Giggs, pia amemsifia sana Rob Swire kwa kusema: “Rob amekuwa Mtumishi mwema mno wa Klabu na yupo hapa muda mrefu. Napenda nimshukuru kwa msaada wake wote na kuniwezesha mimi kucheza kwa muda mrefu. Amefanya kazi bila kuchoka kwa manufaa ya Timu na hajapata hata mapumziko.”

0 comments:

Post a Comment