Tuesday, 27 May 2014

Taifa stars na Malawi leo uwanja wa Taifa

Timu ya Taifa ya Tanzania chini ya kocha mkuu, Mholanzi, Mart Nooij inatarajia kujipima ubavu katika mechi ya kimataifa ya kirafiki jioni ya leo kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam dhidi ya timu ya Taifa ya Malawi (The Flames) kuanzia majira ya saa 11:00 jioni.
Shirikisho la soka Tanzania, TFF kupitia kwa Afisa habari wake, Boniface Wambura imeeleza kuwa,Taifa Stars iliyopiga kambi yake mjini Tukuyu jijini Mbeya itawasili muda wowote kuanzia asuhubi hii majira ya saa 4:00 katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere kwa ndege ya Air Tanzania.
Wapinzani wa Taifa stars tayari wapo jijini Dar es salaam kwa ajili ya mechi hiyo muhimu kwa makocha kuangalia uimara wa timu zao kabla ya kwenda kucheza mechi za mashindano.
Stars na Malawi wanakutana kwa mara ya pili ndani ya mwezi mmoja kwani mei 4 mwaka huu walipambana tena katika uwanja wa Sokoine jijini Mbeya na kutoka suluhu pacha ya bila kufungana.
Mechi hii itatumika na kocha mkuu wa Taifa stars, Nooij, kuangalia kama kuna maboresho katika kikosi chake kinachojiandaa na mechi ya marudiano dhidi ya Zimbabwe mjini Harare.

Malawi (Flames) inayonolewa na mchezaji wake wa zamani Young Chidmozi nayo itakuwa inacheza mechi ya mwisho ya majaribio kabla ya kwenda N’djamena kuikabili Chad.
TFF limewataka watanzania kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu yao ambayo kwa sasa inajengwa upya.
Wambura alitaja kiingilio katika mechi hiyo kuwa kitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa upande wa VIP B na C kiingilio kitakuwa sh. 10,000 wakati kwa VIP A itakuwa ni sh. 20,000.

0 comments:

Post a Comment