Saturday, 5 July 2014

Kagame kuanza Agosti 9 nchini Rwanda

Kikosi cha Vital ' O kilichobeba ubingwa 2013
Michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati maarufu kama CECAFA KAGAME CUP, yataanza huko Kigali Nchini Rwanda kuanzia Agosti 9 na kumalizika Agosti 24.
Akizungumzia hilo Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye amesema Mechi zote zitachezwa Mjini Kigali kwenye Viwanja vya Amahoro na Nyamirambo huku Rubavu ikiwa ni Uwanja wa Akiba.
Vilevile Musonye amesifu Shirikisho la Soka la Rwanda, FERWAFA, na Wizara ya Michezo na Utamaduni ya Rwanda kwa kutoa ushirikiano mzuri na kuandaa mipango mizuri.
Musonye alikumbusha kuwa mara ya mwisho kwa Kagame Cup kufanyika Nchini Rwanda ilikuwa Mwaka 2010 na yalifana sana na kuwa na mafanikio makubwa.
Klabu 4 kutoka Angola, Congo DR na Congo Brazaville huenda zikaalikwa kushiriki michuano hiyo ambayo washiriki wake wa kawaida ni Wanachama wa CECAFA na ambayo tangu Mwaka 2002 Mdhamini wake mkuu ni Rais Paul Kagame wa Rwanda ambae amekuwa akitoa Dola 60,000 kila Mwaka.
Akiongea, Musonye alisema: “Rwanda iko tayari, CECAFA iko tayari na Timu zetu zipo tayari kuja. Tutakuwa na Timu nyingi kwa Mashindano haya kuliko nyuma.”
Musonye alitoa shukrani za dhati kwa Rais Kagame kwa msaada wake.
Vile vile, Musonye amedokeza kuwa Klabu ya Uganda, Sports Club Victoria University, iliyotwaa CECAFA Nile Basin Cup huko Sudan Mwezi uliopita, na AFC Leopards ya Kenya, huenda zikaalikwa kwa kuonyesha ushindani mzuri kwenye Nile Basin Cup ambayo yalikuwa Mashindano mapya ya CECAFA.
Klabu Vigogo za Afrika Mashariki na Kati ambazo zitakuwepo huko Rwanda ni pamoja na KCCA FC ya Uganda, Gor Mahia ya Kenya, Rayon Sport ya Rwanda, Yanga ya Tanzania na Mabingwa Watetezi Vital ‘O kutoka Burundi iliyotwaa Kombe huko Darfur, Sudan Mwaka Jana baada kuibwaga APR ya Rwanda 2-0 kwenye Fainali.
Mashindano haya yatarushwa moja kwa moja kwenye TV na SuperSport International.
Ratiba kamili itatolewa baadae na CECAFA baada Timu zote kuthibitisha kushiriki.
Mbali ya kutwaa Kombe, Bingwa wa Kagame Cup huzoa Donge la Dola 30,000, Mshindi wa Pili Dola 20,000 na Timu ya Tatu hupata Dola 10,000.

0 comments:

Post a Comment